Kamati ya Usimamizi na Uendeshaji wa 
Ligi Tanzania au Kamati ya Saa 72, ilifanya kikao chake juzi Ijumaa 
Aprili 7, 2017 jijini Dar es Salaam na kufikia uamuzi ufuatao. 
Kuhusu Mchezaji Abdi Banda
Mechi namba 194 (Kagera Sugar 2 vs Simba 1). Beki
 wa Simba, Abdi Banda jezi namba 24 amesimamishwa kucheza Ligi Kuu 
wakati akisubiri suala lake la kumpiga ngumi kiungo wa Kagera Sugar, 
George Kavilla jezi namba 15 wakati akiwa hana mpira kusikilizwa na 
kutolewa uamuzi na Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu 
Tanzania (TFF).
Alifanya kitendo hicho ambacho 
hakikuonwa na waamuzi katika mechi hiyo iliyofanyika Aprili 2, 2017 
kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba. Uamuzi wa Kamati umezingatia 
Kanuni ya 9(5) ya Ligi Kuu.
Pia Kamati ilibaini kuwa Banda alifanya 
kitendo cha aina hiyo kwenye mechi namba 169 kati ya Simba na Yanga 
iliyofanyika Februari 25, 2017 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Awali, Klabu ya Kagera Sugar 
iliwasilisha malalamiko dhidi ya kitendo cha beki wa Simba, Abdi Banda 
kumpiga ngumi kiungo wao George Kavilla wakati akiwa hana mpira, na 
Mwamuzi wa mechi hiyo kutochukua hatua yoyote.
Kwa vile kosa hilo ni la kinidhamu, 
Kamati imemsimamisha Abdi Banda kwa mujibu wa Kanuni ya 9(5) wakati 
akisubiri suala lake kusikilizwa na kutolewa uamuzi na Kamati ya Nidhamu
 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF). Kamati ya Nidhamu 
inatarajiwa kukaa wakati wowote wiki ijayo.
Kadhalika Klabu ya Simba iliwasilisha 
malalamiko ikitaka ipewe ushindi wa pointi tatu na mabao matatu kutokana
 na timu ya Kagera Sugar kumchezesha mchezaji Mohamed Fakhi Gharib 
wakati akiwa na kadi tatu za njano katika mechi yao namba 194 
iliyofanyika Aprili 2, 2017 Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.
Kamati baada ya kupitia malalamiko hayo,
 imeahirisha shauri hilo hadi Alhamisi Aprili 13, 2017 kwa vile bado 
inafuatilia baadhi ya vielelezo kuhusu malalamiko hayo kabla ya kufanya 
uamuzi.

0 Komentar untuk "BEKI WA SIMBA ABDI BANDA AMESIMAMISHWA KUCHEZA LIGI KUU"